Blogger Widgets

Monday, September 16, 2013

Kashfa mpya dawa za kulevya

 
 
Na Waandishi Wetu, Mwananchi
Dar es Salaam/Nairobi. Raia wa Nigeria aliyefukuzwa Kenya miezi minne iliyopita kwa kuhusishwa na biashara ya dawa za kulevya, amekamatwa tena nchini humo akiwa na pakiti 425 za heroin, akiaminika kwamba alipitia Tanzania.
Mtu huyo aliyetajwa kwa jina la Enobemhe Emmanuel Peter inaaminika alishukia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam, akitokea Nigeria na kisha kwenda Kenya kwa barabara, kupitia mpaka wa Namanga mkoani Arusha.
Peter alikamatwa pamoja na mwanamke ambaye ni raia wa Kenya, usiku wa Ijumaa iliyopita jijini Nairobi na anatarajiwa kufikishwa mahakamani leo.
Raia huyo wa Nigeria ni kati ya wageni waliofukuzwa nchini humo Juni mwaka huu kwa agizo la Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta aliyeamuru raia wa kigeni wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya wafukuzwe nchini humo.
Mkuu wa Kitengo cha Kupambana na Dawa za Kulevya cha Kenya, Dk Hamisi Massa alisema uchunguzi zaidi wa dawa hizo utafanyika kabla mtuhumiwa huyo kufikishwa mahakamani.
“Ni kati ya watu waliokuwa wamefukuzwa nchini katika nyumba aliyokamatiwa kulikutwa pia na pakiti 425 za heroin,” alisema Dk Massa.
Mtu huyo amekamatwa kutokana na kuwapo kwa taarifa zilizoonyesha kuwa, watu wengi waliofukuzwa Kenya kutokana na kujihusisha na biashara hiyo sasa wamerejea tena.
Julai 9 mwaka huu, Ofisa Uhamiaji wa nchi hiyo, Edward Kabiu Njau alifikishwa mahakamani na kushtakiwa kwa kumruhusu Anaeke Chimenze, aliyefukuzwa nchini humo, kurejea tena.
Chimenze ambaye ni raia wa Nigeria mwenye pasi ya kusafiria namba 02743350, pia anadaiwa kurudi nchini humo kupitia mpaka wa Namanga.
Uhamiaji Tanzania
Msemaji Mkuu wa Idara ya Uhamiaji, Naibu Kamishna, Abbas Irovya alisema hawezi kuzungumzia suala hilo kwa kuwa yupo nje ya ofisi. “Mtafute Tatu ndiye mtu wa habari zaidi, kama atakuwa amepata hizo taarifa atakueleza,” alisema.
Mwananchi ilipomtafuta Tatu Iddi alisema hajapata taarifa hizo na kutaka mwandishi amtumie barua pepe ikiwa na maelezo ya mtu huyo aliyekamatwa ili aweze kutafuta taarifa zaidi.

Naye Kaimu Msemaji wa Idara ya Uhamiaji, Mbaraka Batenga alisema hayuko kwenye nafasi nzuri ya kuzungumzia suala hilo kwa kuwa hakuwa ofisini kutokana na kuugua.
Hata hivyo, alisema kwa kawaida mtu akifukuzwa kwenye nchi moja isitafsiriwe kuwa haruhusiwi kwenda nchi nyingine.
“Naomba nikusaidie kitu kimoja kama kwa ajili ya kuelewa zaidi mambo haya, mtu akifukuzwa kwenye nchi moja haina maana kuwa hawezi kwenda kwenye nchi nyingine,  sisi tukimfukuza mtu itakuwa kosa kama atarudi tena Tanzania,”alisema na kuongeza:
“Kwa hiyo kama huyo mtu alifanya kosa huko Kenya na akafukuzwa Kenya ni kosa kurudi Kenya, hapo hata ofisa aliyemruhusu kurudi huko itabidi akamatwe,” alisema Batenga.
Kwa upande wake, Kamanda wa Kikosi cha Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Godfrey Nzowa alisema mtu akifukuzwa nchi moja haimaanishi kuwa haruhusiwi kwenda nchi nyingine.
Alisema kama kikosi cha kupambana na dawa za kulevya cha Kenya kingekuwa kinashirikiana na kile cha Tanzania, ingekuwa rahisi kuwadhibiti watu hao.
“Wenzetu wangekuwa wanafanya kazi kwa ushirikiano na sisi ingesaidia sana, wakimkamata mtu wanatuambia. Huyo mtu alipita tu Tanzania,” aliongeza Nzowa.
Nzowa alitahadharisha kuwa kumfukuza sio kigezo cha kumzuia mtu kupita Tanzani

0 comments:

Post a Comment