Blogger Widgets

Monday, February 25, 2013

Hivi unajua Wanyakyusa wana asili ya pande mbili - wakati baba akiwa na asili ya Kiluguru na mama Mzulu wa ‘kwa Madiba’. SOMA HAPA UJUE NI KWANINI





Ngoma ya Kinyakyusa
Historia yao

Historia inasema kwamba asili ya Wanyakyusa ni mkoani Morogoro. Kabila hilo likitokana na kabila la Waluguru. Hili hasa ndilo chimbuko la Wanyakyusa.

Inasemekana kwamba mwindaji mmoja wa Kiluguru alitembea peke yake porini bila ya kuongozana na mtu mwingine. Alitembea hadi akafika maeneo ya Kabale huko Suma, Tukuyu wilayani Rungwe. Akiwa huko, akaendelea na kazi yake ya uwindaji.
Baadaye akatokea Mzulu mmoja kutoka Afrika Kusini aliyekuwa na binti yake. Akafika maeneo alikokuwa akiishi yule mwindaji Mluguru, naye akapiga kambi hapo Kabale, wakaungana katika maisha ya uwindaji.

Ikawa kila yule Mluguru akitoka asubuhi kwenda kuwinda, alikuwa akifanikiwa kurejea nyumbani na wanyama wakati rafiki yake wa Kizulu alikuwa akirudi mikono mitupu.

Kutokana na hali hiyo, Mluguru akageuka kuwa mfadhili wa Mzulu, kwa kutoa misaada mara kwa mara, na kwa kulipa fadhila hizo, akamwoza bintiye kwa Mluguru.

Akamwoa na maisha yakaendelea huku nyumbani kwa mwindaji wa Kiluguru na mkewe binti wa Kizulu, kukiwa hakukosekani nyama kama kitoweo.

Kwa sababu ili kuihifadhi nyama ilibidi kwanza ibanikwe, basi kitendo hicho kilisababisha harufu nzuri ya kitoweo kile kusambaa eneo kubwa na kufika hadi ukweni kwake nyumbani kwa Mzulu.

Ndipo Mzulu yule akawa anasema mara kwa mara: “Pale panatoa kyusi kila siku” akimaanisha moshi kwa lafudhi ya lugha ya kwao.

Mazoea ya kutamka ‘kyusi’ kila siku, yakaligeuza neno ‘kyusi’ na sasa likawa linatamkwa ‘kyusa’, baadaye ‘kyusa’ ilipozidi kutamkwa kwa mara nyingi, nayo pia ikabadilika bila kukusudia ndipo watu walipokuwa wakimwita Mluguru ‘Mnyakyusa’, kwa kuwa moshi ukiambatana na harufu ulikuwa ukitokea ndani ya nyumba yake na kusambaa.

Kwa hiyo, tangu hapo na kutokana na jina hilo alilopewa kwa ajili ya mazoea ya kukosea kutamka kitu, hata watoto wake pia waliozaliwa na Mluguru na mkewe Mzulu, wakawa wakiitwa ‘Wanyakyusa’.

Hiyo ndiyo asili na chimbuko la kabila la Wanyakyusa, na kwa kuwa Mnyakyusa alikuwa tayari ana asili ya pande mbili - wakati baba akiwa na asili ya Kiluguru na mama  Mzulu wa ‘kwa Madiba’.

Na hata uchifu ukaanzia mahali pale palipokuwa panaitwa Kabale, na yule Mluguru aliupata uchifu kwa kuwa yeye ndiye aliyekuwa mwanzilishi na mkazi wa kwanza wa eneo lile na ndiye aliyekuwa anafahamika zaidi.

Mavazi yao

Kwa upande wa mavazi, Wanyakyusa walikuwa wakivaa mavazi yaliyokuwa yakijulikana kama ‘Lyabi’, Ni mavazi ya kwanza kwa kabila yakivaliwa enzi za utumwa. Mavazi haya ni yale yanayofunika maeneo ya siri pekee, na kwa wale ‘waheshimiwa’, kidogo basi wao walivaa vazi lililokuwa likiitwa ‘kikwembe’ au ‘kilundo’.

Mavazi haya yaliyovaliwa kwa mtindo kama lubega, ndiyo yaliyomtambulisha na kumtofautisha mhusika mbele ya jamii.

Ngoma yao

Ngoma iliyokuwa ikichezwa na Wanyakyusa enzi hizo, ilikuwa ni ya kuchezea mikuki na mara nyingi ngoma hiyo ilikuwa ikichezwa wakati wa msiba.

Lakini ngoma za kawaida zilizokuwa zikichezwa pasipo kutumia mikuki na wakati wa sherehe na shughuli nyingine, ni  ‘Ipenenga’. Hii mara nyingi ilikuwa ikichezwa na watu ‘wastahiki’ tena kwa madaha na maringo ya hali ya juu. Hata machifu walikuwa wakiicheza sana ngoma hii.

Chakula chao

Chakula chao kikuu na ambacho Mnyakyusa angeonekana kuwa amemkarimu mgeni, si kingine bali ni dizi zinazomenywa na kupikwa maarufu kama ‘mbalaga’.

Mnyakyusa halisi kama atakula chakula lakini akakosa ‘mbalaga’ hujiona kama bado hajakamilisha mlo, ingawaje siku hizi kuna mabadiliko fulani ambayo wengi hupendelea ugali na wali; lakini bado asili ya chakula chao hawawezi kuibadilisha kamwe.

Na ni lazima chakula kama ‘kande’ kipikwe kwenye tukio la msiba uwao wote, kama shughuli za msiba zitakwisha pasipo kupikwa chakula hicho chenye mchanganyiko wa mahindi na maharage; msiba huwa haujakamilika hata kama wafiwa ni watu wenye kujiweza kifedha zaidi lakini ni lazima kande zitapikwa japo kiasi.

Utamaduni wao
Kwa kawaida Wanyakyusa hawana mambo ya unyago kama ilivyo kwa baadhi ya makabila hapa nchini. Wao hawapendelei kabisa mila na desturi za kuwaweka mabinti ndani au kuwafanyia mambo yoyote ya tohara.

Hii ni pamoja na upande wa vijana wa kiume ambao nao hawafanyiwi ya tohara kama makabila mengine isipokuwa tu kwa upande wa vijana wa kiume mara tu wanapotimiza umri wa miaka 13 na kuendelea.

Hawa wazazi wao wa kiume huwatengea eneo ambalo kijana hutakiwa kujifunza kujitegemea akiwa bado mbichi. Hapo hutakiwa kuwa na kibanda chake na kuhama kutoka nyumba moja na wazazi wake.


0 comments:

Post a Comment