Blogger Widgets

Wednesday, March 20, 2013

Wanafunzi washinda danguroni Dar

 
Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Majani ya Chai, Yasinta Assey akionyesha baadhi ya nguo na viatu vya wanafunzi vilivyokutwa katika eneo linalodaiwa kuwa danguro linalotumiwa na wanafunzi wa shule hiyo, jana. Picha na Pamela Chilongola  

Na  Pamela Chilongola, Mwananchi, Dar es Salaam  (email the author)
 
Kwa ufupi
Mkuu wa Sekondari hiyo, Jasinta Assey alikiri na kusema kwamba vitendo vya uvutaji bangi na biashara ya ukahaba kwa wanafunzi wake, vinachangiwa na askari wa Kituo kidogo cha Stakishari ambao alidai wanachukua rushwa kwa wauzaji wa bangi na nyumba bubu za wageni. 
Dar es Salaam. Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Kata ya Majani ya Chai iliyopo Kipawa jijini Dar es Salaam, wametajwa kujiingiza katika kashfa ya ngono, kuvuta na kuuza bangi katika moja ya nyumba zinazozunguka shule hiyo.
Hilo ni tukio lingine jipya, kwani mwishoni mwa mwaka jana, kuliibuka matukio ya ajabu kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi, Ruaruke, Rufiji mkoani Pwani ambao walielezwa kujihusisha na uvutaji bangi hata kukonyeza na kubaka walimu wao.
Mkuu wa Sekondari hiyo, Jasinta Assey alikiri na kusema kwamba vitendo vya uvutaji bangi na biashara ya ukahaba kwa wanafunzi wake, vinachangiwa na askari wa Kituo kidogo cha Stakishari ambao alidai wanachukua rushwa kwa wauzaji wa bangi na nyumba bubu za wageni.

 Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Mkuu wa Shule hiyo, Jasinta Assey alisema ni kawaida ya polisi hao kwenda kwenye nyumba hizo kunakofanyika biashara hizo na kuchukua rushwa badala ya kutatua tatizo.
Alisema ongezeko la utoro katika shule hiyo ni tatizo kubwa na wanafunzi wa kidato cha nne wanaosoma masomo ya sanaa ndiyo wanaoongoza kwa kuvuta bangi na kwenda kufanya ngono katika nyumba zilizo jirani na eneo la shule hiyo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Marietha Minangi alisema hajapata taarifa za hali hiyo.
“Ngoja nimtume Mkuu wa Kituo cha Polisi Stakishari afuatilie kwa karibu,” alisema Minangi na kuongeza: “Lakini ngoja nikwambie, hili suala nakumbuka liliwahi kuripotiwa 2011 wakati nikiwa mkuu wa kituo hicho; nililishughulikia na tulibaini kuwa hakuna mwanafunzi ambaye alikuwa anaenda kwenye nyumba hizo kuvuta bangi wala kufanya ngono.

“Kilichotokea kwa wakati huo ni kwamba, tuliwachukua baadhi ya wanafunzi ili watupeleke mahali walipokuwa wakifanyia vitendo hivyo kutokana na maelezo na vielelezo vyao, lakini hatukubaini hizo sehemu.

“Inawezekana basi haya mambo yameibuka upya baada ya kuona kuna mkuu wa kituo mwingine mpya,” alisema Kamanda Minangi.
Kutokana na matendo hayo, wanafunzi wengi walifanya vibaya mtihani wa kumaliza kidato cha nne mwaka jana.

“Walifeli sana mwaka jana hawa, walimu wapo, tunawapa nyenzo lakini hawataki, ninaiomba Serikali kuingilia kati suala hili kwani ni la muda mrefu na ni faida ya vijana hawa,” alisema.

Shule ya Majani ya Chai ilishika nafasi ya 61 kimkoa kati ya shule 226 wakati ngazi ya taifa, ilishika nafasi ya 543 kati ya shule 3,392.

Wanafunzi 274 walijisajili kufanya mtihani wa kidato cha nne mwaka jana na kati yao 130 walipata sifuri, wakati waliopata daraja la nne ni 85, waliopata Daraja la Tatu ni 18 wakati waliopata daraja la pili ni watano. Hakukuwa na daraja la kwanza na wanafunzi 36 hawakufanya mtihani.

“Baada ya kuona utoro umekithiri shuleni hapo, nilikwenda kutoa taarifa kituo kidogo cha Polisi Stakishari, lakini hawakuonyesha ushirikiano matokeo yake wanakwenda kwa wenyeji hao na kuchukua rushwa.

Hili inaonekana kama ni dili la hawa askari, kwani wapo walionifuata na kunieleza niache kufuatilia, lakini mimi niliwaambia nitafuatilia tu na ilifikia hatua nikatishiwa maisha.
“Baada ya kuona nazidi kutishiwa maisha, niliogopa, nikaacha...na hivi ninavyoongea na wewe, najua tu watanifuata kwani nimeshaambiwa nikipita peke yangu eneo wanakofanyia biashara zao watanifanyia kitu kibaya,
” alisema Assey.

0 comments:

Post a Comment